''Zawadi, Zawadiiii'' ndio maneno yaliyoniamsha asubuhi ya pili.Nilifumbua macho yangu taratibu na kivivu ili kujua aliyekua ananiamsha ni nani. Mama alikua ameinama akinitazama usoni huku mkono wake mmoja ukiwa umenishika begani.
''Mama, shkamoo.'' nilimsalimu kwa sauti ya chini huku nikifumba macho yangu tena. ''Marahaba mwanangu, unaendeleaje?'' aliuliza bila kuondoa mkono wake begani mwangu. ''Nafuu mama! Umekuja na baba?'' swali hilo lilinitoka kabla sijayafumbua macho yangu na kuyaangaza mle chumbani kuona kama baba alikuwapo.
'' Nimekuja nae ila yupo hapo nje anaongea na sijui ndo mwalimu wako yule.Alafu ilikuaje yeye ndo aliyekuleta hospitali , mashoga zako nao wako wapi?'' japo aliuliza kwa sauti ya utaratibu kama kawaida yake nilihisi shauku ya udadisi ndani yake. Nilifikiria kwa sekunde kadhaa nimjibu nini kisha nikamjulisha kwamba niliwaomba watangulie tulipotoka shule na ningeungana nao baada ya kuongea na mwalimu kuhusu mitihani tuliyokua tukitarajia kuanza jumatatu, na nilipokua naongea na mwalimu ndipo nilipoanguka. ''Ahhhh ndo matatizo ya kutokua na pesa haya. Ungeshatibiwa tangu unaanza kujisikia vibaya haya yote yasingetokea.'' Jibu lake lilionyesha kuridhishwa na langu, ila lilinifanya nijihisi kama mkosaji kwa kumfanya mama ajione kama mzazi asiyeweza kutosheleza mahitaji ya mwanawe, hata pale anapokua mgonjwa. Nilitamani kutoa maneno ya kumfariji ila kabla sijafanya hivyo mlango uligongwa na kufunguliwa mara hiyo hiyo.
Wa kwanza kuingia alikua baba aliyekua amevalia kama ambavyo hua anavaa siku zote akielekea kwenye shughuli zake , kaptula, shati na ndala chakavu kiasi.Bila kusahau kofia yake chakavu aliyotumia kujikinga na jua. Japo kua ilikua imetoboka sehemu kadhaa juu na pembeni bado aliivaa kila siku. Rangi yake ya kijani ilikua imefifia kana kwamba ilikua imedumbukizwa kwenye jiki kwa nia ya kupoteza rangi yake ya awali . Nyuma yake alifuatiwa na mwalimu kisha daktari yule mrembo aliyenihudumia jana yake.
''Hujambo mama?” alinisalimu baba kabla sijatoa shikamoo niliyokua najiandaa kumpa. “Salama tu shikamoo baba!” nilimjibu huku nikimtazama ili niweze kumsoma alikua katika hali gani. Uso wake ulionyesha kuchoka kama ulivyokua wa mama ila alijitahidi kutabasamu hivyo nikajua alikua sawa.
Mwalimu yeye alisimama karibu kabisa na mlango huku akimtazama daktari ambae kwa wakati ule alikua akinipima. “Mrembo naomba uvute hewa ndani kwa sekunde chache kabla ya kuiachia kisha usubiri tena kwa sekunde chache kabla ya kuvuta tena ndani.” maagizo hayo ya daktari yaliambatana na mkono wake mmoja ukisogeza kifaa chake kila kona ya kifua changu upande wa kushoto huku mwingine ukiwa umekishikilia kilipoishia sikioni mwake.
“Mapigo ya moyo yako normal, sasa ngoja niongee na wazee kidogo .Nikirudi nikute bado unapumua ehhhh!!!.” aliniambia mimi uso wake ukiwa umejaa tabasamu lililoonyesha meno yake meupe yaliyojipanga vyema kabla ya kugeuka walipokua wamesimama baba na mama na kuwaomba wamfuate. “Kama hamtojali naomba twendeni ofisini tukaongee kidogo.”